Paulo Au Yesu?


Hebu yazingatie Mahubiri ya Yesu aliyotoa juu ya Mlima wa Zaituni:

Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii;  la, sikuja kutangua, bali kutimiliza.  Kwa maana, amin, nawaambia, Mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka, yodi moja wala nukta moja ya torati haitaondoka, hata yote yatimie. Basi mtu ye yote atakayevunja amri moja katika hizi zilizo ndogo, na kuwafundisha watu hivyo, ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni;  bali mtu atakayezitenda na kuzifundisha, huyo ataitwa mkubwa katika ufalme wa mbinguni. Maana nawaambia ya kwamba, Haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni.
Mathayo 5.17-20

Mnamo mahubiri ya Mlima wa Zaituni ndio yanapatikana mafunzo makubwa ya Yesu Kristo.  Tunaweza kusema kuwa humu, khasa, ndio umo Ukristo;  yaani ikiwa tunaamini ya kuwa Yesu ndiye Katika kifungu cha maneno hayo tuliyoyanukulu ya Yesu tunaona ya kuwa ni muhali mtu kuingia katika ufalme wa mbinguni, yaani Peponi, mpaka haki ya mtu izidi ile ya waandishi na Mafarisayo. Yaani wema uutendao uzidi ule wa wanazuoni wa Kiyahudi.  Ni nini hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo?  Ni kuifuata sharia ya Taurati neno kwa neno, na pia waliofunza manabii wengineo. 

Ndio maana Yesu akasema: 

"Msidhani ya kuwa nalikuja kutangua torati au manabii, sikuja kutangua, bali kutimiliza."

Kazi yake haikuwa kutengua sharia ya Taurati na kuleta kitu kingine cha kutengua au kugonganisha na mafunzo ya sharia ya Mwenyezi Mungu na Mitume wake, bali kaja yeye kutimiliza kwa kuwafunza Mayahudi umuhimu wa mambo ya kiroho katika sharia. Kutii madhaahiri ya sharia tu na kuwacha undani wake, uchamngu, hakutoshi. Mwenyezi Mungu atiiwe kwa dhaahiri na kwa siri.  Yesu alishikilia sana kufundisha na kutenda, aliposema: 

"Basi mtu ye yote atakayevunja amri moja katika hizi zilizo ndogo, na kuwafundisha watu hivyo, ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni;  bali atakayezitenda na kuzifundisha, huyo ataitwa mkubwa katika ufalme wa mbinguni."

Katika amri za Taurati ni kama hii iliyomo katika Biblia:

Na nguruwe, kwa sababu yeye anazo kwato ni mwenye miguu iliyopasuka kati, lakini hacheui, yeye ni najisi kwenu. Msile nyama yao, wala msiiguse mizoga yao;  hao ni najisi kwenu.
Mambo ya Walawi 11.7-8

Kwa hiyo naliwaambia wana wa Israeli, Msile damu ya mnyama wa aina yo yote; kwa kuwa uhai wa wanyama wote ni katika hiyo damu yake;  atakayeila awaye yote atakatiliwa mbali.  Tena kila mtu atakeykula nyamafu, au nyama aliyeraruliwa na wanyama, kama ni mzalia, kama ni mgeni, atafua nguo zake, na kuoga majini, naye atakuwa najisi hata jioni;  ndipo atakapokuwa safi.
Walawi 17.14-15

Hizo ni amri ziliomo katika Taurati, sharia ya Mungu, ambayo Yesu amesema kama ilivyo katika Injili ya Mathayo kuwa mwenye kuivunja ndogo yao na akawafundisha watu hivyo basi ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni. 

Na kuvunja hayo khasa ndio Paulo kafundisha. Msikieni:

Kila kitu kiuzwacho sokoni kuleni, bila kuuliza-uliza, kwa ajili ya dhamiri;  maana Dunia ni mali ya Bwana na vyote viijazavyo.
1 Wakorintho 10.25-26

Mnamwona Paulo anavyobomoa sharia ya Taurati  waliyoifwata Manabii wote, hata Yesu na wanafunzi wake thenashara, ya kuwa kuna vyakula vilivyo halali na kuna vingine ni najisi, haramu kuliwa, kama nguruwe, vya kunyongwa na damu?  Yesu kafunza nini, na Paulo anafunza nini!

Katika waraka wake aliowapelekea Wagalatia Paulo anasema:

Mmetengwa na Kristo, ninyi mtakao kuhesabiwa haki kwa sheria; mmeanguka na kutoka katika hali ya neema, Maana sisi kwa Roho tunalitazamia tumaini la haki kwa njia ya imani. Maana katika Kristo Yesu kutahiriwa hakufai neno, wala kutokutahiriwa, bali imani itendayo kazi kwa upendo.
Wagalatia 5.4-6

Kwa kauli moja Paulo ameitengua sharia yote. Yesu kasema nini juu ya Mlima wa Zaituni na Paulo anasema nini katika barua yake kwa Wagalatia?  Yesu alifuata sharia ya Mwenyezi Mungu na aliihishimu na akaahidi kuwa yeye hatoitengua kabisa, ila ataitimiza. Paulo anaibeza sharia na kuiona kuwa ni laana. Yesu akila kilicho halalishwa na Mungu, na alikiepuka kilicho harimishwa na Mungu. Paulo anatwambia tule kila kiuzwacho sokoni bila ya kujali dhamiri yetu. 

Yesu na Manabii wote tangu Nabii Ibrahim walitahiriwa kwa kufuata amri ya Mungu kama isemavyo Biblia:

Mungu akamwambia Ibrahimu, Nawe ulishike agano langu, wewe na uzao wako kwa vizazi vyao baada yako.  Hili ndilo agano langu utakalolishika, kati ya mimi na wewe, na uzao wako baada yako, Kila mwanamume wa kwenu atatahiriwa.
Mwanzo 17.9-10

Paulo mjuaji, anasema kumpinga Mungu:
Kwa sababu kutahiriwa si kitu, wala kutokutahiriwa, bali kiumbe kipya.
Wagalatia 6.15

Katika barua yake aliyowapelekea Warumi ndio kabisa Paulo anaiangamiza sharia ya Mungu na kufanya vitendo kuwa havina maana yo yote.Chenye maana peke yake ni imani tu.

Basi, twaona ya kuwa wanadamu huhesabiwa haki kwa imani pasipo matendo ya sheria.
Warumi 3.28

Kwa Paulo kuamini kuwa Yesu kafa msalabani na damu yake kuwa ni fidia kwa dhambi zetu ndio kwenye maana, sio kufuata sharia wala vitendo.  Kwake yeye ile Taurati, ambayo Yesu mwenyewe hakuja kuitengua bali kaja makusudi kuitimiza, ni kifungo na pingamizi.

Anawaambia Warumi:

Bali sasa tumefunguliwa katika torati, tumeifia hali ile iliyotupinga, ili sisi tupate kutumika katika hali mpya ya roho, si katika hali ya zamani, ya andiko.
Warumi 7.6

Paulo anaiona Taurati ni kifungo, pingamizi, bali ni laana. Hayo sio maoni ya Yesu ambaye amesema:
 "Mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka, yodi moja wala nukta moja ya torati haitaondoka."

·         Je, kwa kuingia Paulo katika umoja wa Kikristo ndio tusema mbingu na nchi zimeondoka? 
·         Au kwa kutundikwa Yesu msalabani (ikiwa kweli katundikwa) ndio tuseme mbingu na nchi zimeondoka?
·         Mbona watu wameyasahau upesi maneno ya Yesu mwenyewe, na kuyasikiliza ya Paulo? Kwa sababu yanakubaliana na matamanio yao? 

Mafunzo ya Paulo yalileta mzozano na ubishi mkubwa tangu pale mwanzo katika historia ya Kanisa baina ya kikundi chake cha Wakristo waliomfuata kutoka upagani, na wale Wakristo wa asli ya Kiyahudi.  Wao walipinga moja kwa moja ile shauri ya kwenda kupelekewa mafunzo ya Ukristo mataifa waliokuwa hawakutahiriwa, wala hawaikubali sharia ya Taurati.  Baadhi ya wanafunzi wa Yesu walikuwa hawakubali hata kula nao wale "
wasiotahiriwa".  Wao walikuwa wanajua vyema kuwa Yesu aliwakataza wasend kuwahubiria mataifa mengine isipokuwa Mayahudi tu, kwani ni wao ndio walikuwa wanaamini Mungu Mmoja na wao ndio wakiifuata sharia ya Mungu. Mwishoe ulifanywa mkutano na yakawapo baadhi ya masikilizano kuwa yafaa kuhubiriwa Ukristo kwa mataifa yasiokuwa ya Kiyahudu, na wao wasilazimishwe kubeba mizigo mizito katika dini kama vile wenye asli ya Kiyahudi.  Walitumwa Paulo na Barnaba kuwaendea hao mataifa, nao ni Wazungu wa Kirumi na Kigiriki, na wakachukua barua iliomalizikia maneno haya muhimu:

Kwa maana ilimpendeza Roho Mtakatifu na sisi, tusiwatwike mzigo ila hayo yaliyo lazima, yaani, mjiepushe na vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na damu, na nyama zilizosongolewa na uasherati.  Mkijizuia na hayo mtafanya vema. Wasalamu.
Matendo 15.28-29

Nyama zilizosongolewa, yaani nyama za kunyonga, zisiochinjwa. Yazingatieni haya si maamrisho ya Yesu, lakini ni masikilizano baina akina Paulo na wanafunzi wake Yesu, (kwa ridhaa ya Roho Mtakatifu) baada ya kuwa Yesu mwenyewe hayupo tena. Ikiwa hayo ndiyo waliokubaliana ilikuwaje Paulo tena kuwaandikia Wakorintho:

"Kila kitu kiuzwacho sokoni kuleni bila ya kuuliza-uliza, kwa ajili ya dhamiri" (?)

Lakini Paulo ni Paulo.
Mtakatifu Paulo anadai kuwa yeye aliteuliwa makhsusi kuwa ni mtume wa Yesu katika ufunuo (Wahyi), na kuwa bado yeye anaendelea kupata amri moja kwa moja kutokana na mwenyewe Bwana Yesu, ijapokuwa amri hizo na mafunzo hayo yanapingana kabisa na yale waliyoyapata wale wanafunzi wake Ysu waliokuwa naye mwenyewe alipokuwa hai. Yeye Paulo hakupata kuonana na Yesu, bali yeye alikuwa ni mpinzani mkubwa wa Ukristo na akawa ni sababu ya kuteswa na kuuwawa Wakristo kadhaa wa kadhaa, mmoja wao ni Mtakatifu Stefano, shahidi wa mwanzo katika Wakristo. Paulo alikuwa na asli ya Kiyahudi, na dini yake rasmi ilikuwa ya Kiyahudi. 

Kwa kuwa alizaliwa nje ya Palastina katika mamlaka ya Kirumi alikuwa na uraia kamili wa Kirumi, na huko alipata fursa ya kusoma ilimu na falsafa za Kiyunani.  Mazingara yake yote ya Kigiriki na Kirumi yalikuwa ya kikafiri, kipagani.  Kwani Magiriki na Warumi walikuwa washirikina wenye kuamini chungu ya miungu, kama ilivyokuwa ada ya karibu mataifa yote ya wakati ule isipokuwa Mayahudi. Yalipozuka mafunzo ya Yesu Kristo, ambayo kwa asli yake hayakuwa ila ni kuendeleza ile ile imani ya Kiyahudi ya Mungu Mmoja na kufuata sharia ya Taurati na kuongeza uchamngu, na ikawa mafunzo hayo yanaendelea juu ya kupingwa, Paulo aliona anaweza kuipa nguvu hiyo dini au kwa hakika madhehebu mpya kwa kuwatia wale Warumi na Magiriki kwa kuchanganya imani zao na falsafa zao pamoja na imani ya Kiyahudi.  Mayahudi wanaamini Mungu Mmoja, ndio.

Ukristo unaamini Mungu Mmoja.  Magiriki na Warumi wanaamini miungu mingi, si chini ya watatu, ndio na Ukristo nao unaamini hivyo. Jee, si pana mgongano hapo? La, katika Ukristo imani ni ya Mungu Mmoja katika Utatu Mtakatifu: Mungu Mmoja, mwenye nafsi tatu, Baba, Mwana na Roho Mtakatifu.

Mapagani wa Kigiriki na Kirumi wakiamini mungu aliyekufa, akafufuka na akapaa mbinguni. Hilo si kitu wanaweza kuendelea na imani hiyo katika Ukristo. Wazungu magovi hawataki kutahiriwa. Hapana kitu, kutahiriwa si kitu wala kutotahiriwa. Hoja ipatikane tahara ya roho.

Wazungu wamezoea kula kila kitu, nguruwe, damu, kilichochinjwa na kisichochinjwa. Hilo si tatizo, mtaendelea vivyo hivyo, kwani dhambi ni kitokacho mdomoni, sio kiingiacho.  Kuleni kila kiuzwacho sokoni. Hapana halali wala haramu.  Huo ndio Ukristo mpya wa Paulo, na hiyo ndio Thiolojia yake ambayo, inasikitisha Wakristo wameifuata, wakayaacha mafunzo mepesi na yaliyonyooka ya mwenyewe Yesu Kristo.

Hayo ni maji makuu, letu sisi ni kuangalia yaliyomo ndani ya Biblia Takatifu. Tuiache hiyo iseme.  Khabari za kugeuka Paulo akaacha kumpinga Yesu, na badala yake akawa mfuasi wake zinasimuliwa pahala patatu katika Matendo ya Mitume katika Agano Jipya la Biblia. Na katika zote mara tatu kisa hicho kinakhitalifiana katika mambo muhimu. Kwanza tunasoma katika Sura ya 9 mstari wa 3 mpaka wa 7:

Hata (Paulo) alipokuwa akisafiri, ikawa anakaribia Dameski; ghafula ikamwangaza kote kote nuru kutoka mbinguni. Akaanguka chini, akasikia sauti ikimwambia, Sauli, Sauli, (yaani Paulo) mbona waniudhi?  Akasema, U nani wewe, Bwana?  Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe.  Lakini simama, uingie mjini, nawe utaambiwa yakupasayo kutenda.  Na wale waliosafiri pamoja naye wakasimama kimya, wakiisikia sauti, wasione mtu.
Matendo 9.3-7

Katika maelezo hayo hapo ni mwandikaji anasimulia. Yapo mambo mane lazima tuyazingatie vizuri katika maelezo hayo:
  1. Mwangaza ambao Paulo ulimwangaza.  Haikusemwa kuwa wengine waliuona mwangaza ule au la, lakini waliisikia sauti.
  2. Ni Paulo ambaye "akaanguka chini."
  3. Yeye na wale watu waliokuwa pamoja naye waliisikia sauti, lakini hawakumwona mtu.
  4. Sauti ya Yesu ilimuamuru "aingie mjini, naye ataambiwa yampasayo kutenda."  Hapo hakuambiwa nini la kutenda.
 Katika Biblia hiyo hiyo, katika kitabu hicho hicho cha Matendo ya Mitume, sura 22, mstari wa 6 mpaka wa 10 ipo ncha ya pili ya hadithi kusimulia tukio lile lile. Msimulizi hapa ni Paulo mwenyewe:

Ikawa nilipokuwa nikisafiri, nikikaribia Dameski, wakati wa adhuhuri, ghafula nuru kuu ilitoka mbinguni, ikanimulikia pande zote. Nikaanguka nchi (yaani chini), nikasikia sauti ikiniambia, Sauli, Sauli, mbona unaniudhi?  Nikajibu, Wewe u nani, Bwana?  Akaniambia, Mimi ni Yesu Mnazareti, ambaye wewe unaniudhi.  Na wale waliokuwa pamoja nami waliiona ile nuru, lakini hawakuisikia ile sauti ya yule aliyesema nami. Nikasema, Nifanye nini, Bwana?  Bwana akaniambia, Simama, uingie Dameski, na huko utaambiwa habari za mambo yote yaliyoamriwa uyafanye.
Matendo 22.6-10

Ncha hii yakubaliana na ile ya mwanzo katika mambo haya:
  1. Aliyeanguka chini ni Paulo na sio wale waliokuwa pamoja naye.
  2. Aliloambiwa Paulo ni kuingia mjini na huko ndiko atakoambiwa nini la kulifanya.
 Ncha hii lakini inakosana na ile ya kwanza kuwa ya kwanza yasema ya kuwa wale waliokuwa naye "wakasimama kimya, wakisikia sauti, lakini haikusema kuwa waliona nuru."

Katika ncha hii ya pili twaambiwa: waliiona ile nuru, lakini hawakuisikia ile sauti.
Ncha ya tatu  ya tukio hilo hilo muhimu kabisa katika historia ya Ukristo inaelezwa katika maneno yake mwenyewe Paulo vile vile kama inavyosimuliwa katika kitabu kile kile cha Matendo ya Mitume sura ya 26 mstari wa 12 mpaka wa 18:

Basi katika kazi hiyo nilipokuwa nikienda Dameski, mwenye mamlaka na maagizo ya wakuu wa makuhani;  Ee Mfalme, ndipo wakati wa adhuhuri njiani naliona nuru inatoka mbinguni ipitayo mwangaza wa jua, ikinimulikia mimi, na wale waliofuatana nami pande zote. Tukaanguka nchi (chini) sote, nikasikia sauti ikisema nami kwa lugha ya kiebrania, Sauli! Sauli!  Mbona waniudhi? ni vigumu kwako kuupiga mateke mchokoo (ujiti wenye ncha wa kuchokolea). Nami nikasema, Wewe u nani, Bwana? Bwana akaniambia, Mimi ni Yesu, ambaye wewe unaniudhi.  Lakini inuka, usimame kwa miguu yako, maana nimekutokea kwa sababu hii, nikuweke wewe uwe mtumishi na shahidi wa mambo haya uliyoyaona, na wa mambo ambayo katika hayo nitajidhihirisha kwako;  nikikuokoa na watu wako, na watu wa Mataifa, ambao nakutuma kwao;  uwafumbue macho yao, na kuwageuza waiache giza na kuielekea nuru, waziache na nguvu za Shetani na kumwelekea Mungu; kisha wapate msamaha wa dhambi zao, na urithi miongoni mwao waliotakaswa kwa imani iliyo kwangu mimi.
Matendo 26.12-18

Sasa hapa tunaona khitilafu kubwa na zile ncha za hadithi ziliomo katika sura ya 9 na sura ya 22 katika hicho hicho kitabu kimoja cha Matendo ya Mitume. Hebu tuchungue:
  1. Kwa mujibu wa ncha hii si Paulo pekee aliyeona nuru - kama ilivyoelezwa pale mara ya kwanza - lakini wote waliokuwa naye waliona nuru, kama ilivyoelezwa mara ya pili.
  2. Hapa Paulo anasema: Tukaanguka nchi sote. Haya yanapinga ncha ya kwanza na ya pili zilizosema kuwa ni Paulo tu peke yake ndiye aliyeanguka chini.
  3. Katika masimulizi ya kwanza na ya pili ilisemwa wazi kuwa Paulo aliambiwa aingie mjini Demeski na huko ataambiwa habari za mambo yote yaliyoamriwa ayafanye.  Hii mara ya tatu mambo yote ameamuriwa hapo hapo kabla ya kuingia mjini, kinyume na ilivyosimuliwa mara ya kwanza na ilivyosimuliwa mara ya pili. Tena hapo Paulo alimsikia Yesu anamuamrisha amri kinyume na alivyokuwa akiwafunza na kuwaamrisha wanafunzi wake siku zote katika uhai wake - anamuamrisha Paulo apeleke utume wa Yesu kwa mataifa mengine yasiyokuwa Mayahudi. Kadhaalika kinyume na mafunzo ya Yesu katika uhai wake anamuamrisha afunze kuhesabiwa haki kwa imani na kufutiwa dhambi.
 Ni wazi kuwa Paulo kabla ya kutanasari kwake alikwisha jitayarisha namna gani atavyougeuza Ukristo wa Yesu, waliokuwa wakiujua wote wanafunzi wake kumi na mbili, uwe Ukristo wake yeye Paulo.

Na kwa nini Paulo aliongeza mengi aliposimulia mara hii ya tatu kuliko ilivyosimuliwa zile mara mbili za mwanzo?  Ni kwa sababu hapa anasema na Mfalme Agripa.  Lakini yafaa tusite na tujiulize:
 Nini thamani ya shahidi anayetoa ushahidi wake kwa polisi, akaubadilisha kidogo akifika kwa hakimu, na akatoa hadithi nyengine kabisa anapofika mahkama kuu kwa jaji?  Hapana awezae kumueleza Paulo alivyo kama alivyojieleza mwenyewe katika barua yake aliyowapelekea Wakorintho.

Amesema:
Maana, ingawa nimekuwa huru kwa watu wote, nalijifanya mtumwa wa wote, ili nipate watu wengi zaidi.  Nalikuwa kama Myahudi kwa Wayahudi, ili niwapate Wayahudi;  kwa wale walio chini ya sheria, nalikuwa kama chini ya sheria, (ingawa mimi mwenyewe si chini ya sheria,) ili niwapate walio chini ya sheria.  Kwa wale wasio na sheria nalikuwa kama sina sheria, (si kwamba sina sheria mbele za Mungu, bali mwenye sheria mbele za Kristo), ili niwapate hao wasio na sheria.  Kwa wanyonge nalikuwa mnyonge, ili niwapate wanyonge. Nimekuwa hali zote kwa watu wote, ili kwa njia zote nipate kuwaokoa watu.
1 Wakorintho 9.19-22

Yaweza kuwa ni kweli kuwa mwenyewe Paulo akiamini kuwa hila hizo zote azitendazo ni kwa ajili apate "kuwaokoa watu."  Wengi miongoni mwa wataalamu wa Biblia wanakubaliana na Dr. Craveri na Dr. Schonfield kuwa makusudio ya Paulo ni kuwa apate yeye binafsi wafuasi wengi zaidi ili apate kuwashinda wale wanafunzi wa Yesu mwenyewe. Kwa hivyo ndio akawa hasikii haoni. Kwa lengo hilo yu tayari kufanya lo lote, hata akakhiari kugeuza mafunzo ya Kristo ili apate wafuasi yeye "kwa jina la Kristo." Kwa hakika wale wafuasi wake kutokana na mataifa walibakia kuwa vile vile makafiri ila waligeuzwa jina tu, wakaitwa Wakristo.

Ndio hivyo alivyowaandikia Warumi:
Lile neno li karibu nawe, katika kinywa chako, na katika moyo wako:  yaani, ni lile neno la imani tulihubirilo.  Kwa sababu, ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka.
Warumi 10.8-9

Ndio hivyo Ukristo umerahisishwa na Paulo ili isiwe taabu kwa makafiri waweze kuitwa Wakristo bila ya kuufuata Ukristo wa Yesu. Katika mtindo huu Paulo alipata upinzani kutokana na wengi, kama tunavyoona katika waraka wa Yakobo, nduguye Yesu, unavyofunza imani ya matendo, si imani tupu.

Natusome:
Ndugu zangu, yafaa nini, mtu akisema ya kwamba anayo imani, lakini hana matendo?  Je! ile imani yaweza kumwokoa?  Ikiwa ndugu mwanamume au ndugu mwanamke yu uchi na kupungukiwa na riziki, na mtu wa kwenu akawaambia, enendeni zenu kwa amani, mkaote moto na kushiba, lakini asiwape mahitaji ya mwili, yafaa nini?  Vivyo hivyo na imani, isipokuwa ina matendo, imekufa nafsini mwake.  Lakini mtu atasema, Wewe unayo imani, nami ninayo matendo. Nionyeshe imani yako pasipo matendo, nami nitakuonyesha imani yangu kwa njia ya matendo yangu. Wewe waamini ya kuwa Mungu ni mmoja;  watenda vema. Mashetani nao waamini na kutetemeka.  Lakini wataka kujua, wewe mwanadamu usiye kitu, kwamba imani pasipo matendo haizai? Je!  baba yetu Ibrahimu hakuhesabiwa kuwa ana haki kwa matendo, hapo alipomtoa Isaka mwanawe juu ya madhabahu? Waona kwamba imani ilitenda kazi pamoja na matendo yake, na ya kwamba imani ile ilikamilishwa kwa njia ya matendo yale. Maandiko yale yakatimizwa yaliyonena, Ibrahimu alimwamini Mungu, ikahesabiwa kwake kuwa ni haki;  naye aliitwa rafiki ya Mungu. Mwaona kwamba mwanadamu huhesabiwa kuwa ana haki kwa matendo yake;  si kwa imani peke yake.  Vivyo hivyo na Rahabu, yule kahaba naye, je! Hakuhesabiwa kuwa ana haki kwa matendo, hapo alipowakaribisha wajumbe, akawatoa nje kwa njia nyingine?  Maana kama vile mwili pasipo roho umekufa, vivyo hivyo na imani pasipo matendo imekufa.
Yakobo 2.14-26
Mafunzo haya yanapingana moja kwa moja na yale ya Paulo, na yanakubaliana moja kwa moja na yale ya Yesu, mwenyewe.  Si ajabu basi kumsikia Paulo anakakamia kwa hasira isiyofichikana akisema:
Lakini nifanyalo nitalifanya, ili niwapinge hao watafutao nafasi wasipate nafasi;  ili kwamba katika neno hilo wajisifialo waonekane kuwa kama sisi.  Maana watu kama hao ni mitume wa uwongo, watendao kazi kwa hila, wanaojigeuza wawe mfano wa mitume wa Kristo.   Wala si ajabu.  Maana Shetani mwenyewe hujigeuza awe mfano wa malaika wa nuru. Basi si neno kubwa watumishi wake hao wakajigeuza wawe mfano wa watumishi wa haki, ambao mwisho wao utakuwa sawasawa na kazi zao.
2 Wakorintho 11.12-15

Ni dhaahiri kuwa Paulo anakusudia kwa matusi yake haya kuwatukana wale wanafunzi wa Yesu, ambao Yesu mwenyewe aliwateua, ambao wakiongozwa katika kutimiliza ujumbe wa Yesu na watu kama Yakobo, ambaye anaambiwa kuwa ni nduguye Yesu.

Je, sisi tutendeje tunapokabiliwa na maoni mbali mbali yanayogongana miongoni mwa watu ambao wote wanadai kuwa ni wanafunzi wa Yesu, ijapokuwa huyu mmoja Paulo, hata hakumwona Yesu, na huo ushahidi wa kuwa kamwona katika njozi ni wake yeye tu, tena unagongana na kupingana wenyewe kwa wenyewe?  Tutendeje?

Liliopo ni tuyaendee mafunzo yake mwenyewe Yesu, ambayo ijapokuwa yametatanishwa na maongezo na mapunguzo, lakini hayaachi kuwepo ya kutosha kwa jumla kutufahamisha nini khasa mafunzo yake.  Ikiwa kweli tunatafuta hakika ya mambo na ukweli wake basi tutayachukua yale yalio wazi, dhaahiri, katika maneno yake mwenyewe Yesu, na tusiyabali yale ambayo ni maneno ya wasimulizi.  Kadhaalika yasitushughulishe yale ya mafumbo yanayotatanisha tukajaribu kuleta tafsiri na maelezo tuyapendayo nafsi zetu.  Ikiwa ni kufasiri basi tufasiri fumbo kwa kauli ya Yesu ilio wazi. Wapotoshaji hufanya kinyume cha hayo.

Mafundisho yaliyotulia kabisa ya Yesu ni yale aliyohubiri juu ya Mlima wa Zaituni.  Na maoni yake yaliyo wazi na kauli ya kukata juu ya sharia na matendo, ni yaliyomo katika sura 5 ya Mathayo. Akizungumzia juu ya wale wanaodai kuwa wao ni wafuasi wake, na kuwa ati wanafunza mafunzo yake, na huku kumbe wanayapotoa yale aliyoyafunza, Yesu anaambiwa kasema:

Si kila mtu aniambaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni;  bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni.   Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi?  Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.  Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba;  mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile isianguke;  kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba.  Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga;  mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka;  nalo anguko lake likawa kubwa.
Mathayo 7.21-27

Hayo ni maneno aliyokhitimishia Yesu mawaidha yake juu ya Mlima wa Zaituni.  Ni maneno yaliyokaa sawa, yawazi, hayana ubabaishi.  Ni nani hao "watendao maovu", hao wapumbavu, wasiofuata mafunzo ya Yesu wakayatenda, mafunzo ambayo msingi wake ni kutimiliza sharia na manabii, na kutenda mapenzi ya Mungu?  Ni nani hao wanaodai kufanya miujiza na kuponyesha watu kwa jina la Yesu, na kudai kuwa ni mitume wa Kristo, na huku wanapinga mafunzo yake, na kuwaambia watu kuwa wataokoka kwa imani tu kwamba Yesu kafa msalabini kwa ajili yao, bila ya haja ya vitendo?  Ni nani hao wanaolitumia jina la Yesu naye mwenyewe atawakataa?  Kama tuna akili basi yafaa tuitumie.  Tusiwe kama mtu mpumbavu ajengaye nyumba yake juu ya fungu la mchanga.  Tutaanguka, na anguko letu litakuwa kubwa.

Mafunzo ya Yesu Kristo si haba, lakini kwa ufupi wa maisha yake (aliwahi kuhubiri kiasi miaka miwili mitatu tu) na kutokuwa tayari ulimwengu kuchukua kweli yote, hakuweza kutimiza ujumbe wote wa Mwenyezi Mungu.  Ni hikima yake Mwenyezi Mungu kuwa kila nabii aliyemleta alikuwa anaongeza juu ya yale yaliyotangulia.  Ni kweli Yesu alisema kama ilivyo katika Mathayo 5.17-20 ambayo tumekwisha yataja kuwa yeye alikuja kutimiza Taurati na mafunzo ya Manabii, hakuja kutengua lo lote katika hayo.  Ulipokaribia wakati wake wa kuondoka aliungama kuwa mengi aliyo nayo hana nafasi ya kuyasema, lakini atakuja mwenginewe ambaye atauwongoza ulimwengu kwenye kweli yote, na ataufundisha ulimwengu mafunzo kaamili juu ya dhambi na haki.

Injili ya Yohana inanukulu maneno ya Yesu:
Lakini sasa mimi naenda zangu kwake yeye aliyenipeleka, wala hakuna mmoja wenu aniulizaye, Unakwendapi?  Ila kwa sababu nimewaambia hayo huzuni imejaa mioyoni mwenu.  Lakini mimi nawaambia iliyo kweli;  yawafaa ninyi mimi niondoke;  kwa maana mimi nisipoondoka, huyo Msaidizi hatakuja kwenu;  bali mimi nikenda zangu, nitampeleka kwenu.  Naye akiisha kuja, huyo atauhakikisha ulimwengu kwa habari ya dhambi, na haki, na hukumu.  Kwa habari ya dhambi, kwa sababu hawaniamini mimi; kwa habari ya haki, kwa sababu mimi naenda zangu kwa Baba, wala hamnioni tena;  kwa habari ya hukumu, kwa sababu yule mkuu wa ulimwengu huu amekwisha hukumiwa.  Hata bado nikali ninayo mengi ya kuwaambia,  lakini hamwezi kuyastahamili hivi sasa. Lakini yeye atapokuja huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote;  kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe lakini yote atayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake.  Yeye atanitukuza mimi; kwa kuwa atatwaa katika yaliyo yangu na kuwapasha habari.
Yohana 16.5-14

Kwa mujibu wa maneno hayo kama ilivyo katika Injili ya Yohana, Yesu anawaambia wanafunzi wake kuwa yeye yu karibu kuondoka duniani, na ya kwamba hajatimiza ujumbe wake, lakini atakuja mwenginewe ambaye ameitwa majina mbali mbali kwa mujibu wa tafsiri mbali mbali za Biblia.  Hapa anaitwa Msaidizi katika tafsiri hii ya Kiswahili inayoitwa Union Version.  Kwa mujibu wa tafsiri ya zamani ya Kiingereza, King James's Authorised Version, anaitwa Comforter, yaani Mliwazi;  na kwa mujibu wa tafisiri nyengine ya Kiingereza ya kisasa Revised Standard Version, anaitwa Counsellor, yaani Mshauri, na tafsiri nyengine mpya mpya za Kiingereza anaitwa Helper, ambayo maana yake pia ni Msaidizi. Tafsiri ya Kiarabu ya Darul Kitabul Muqaddas ya Cairo anaitwa Al Mu'azzi yaani Mliwazi.  Vyo vyote vile iwavyo huyo Msaidizi, au Mliwazi, au Mshauri, ameelezwa na Yesu kwamba:
  1. Atakuja baada yake Yesu, yaani wakati huo hayupo;
  2. Atauhakikisha ulimwengu kwa habari ya dhambi, na haki na hukumu;
  3. Atauongoza ulimwengu autie kwenye kweli yote;
  4. Hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini atakayoyasikia atayanena;
  5. Atatoa khabari ya mambo yajayo;
  6. Atabakia nasi milele;
  7. Atamtukuza Yesu Kristo.
 Hebu natuichungue bishara hii ya Yesu bila ya chuki, bila ya mapendeleo, na bila kutiwa pingu na mawazo tuliyofungwa nayo tangu utotoni.  Sasa tu watu wazima na tuna akili zetu, natuzitumie. Wakristo wengi wanachukulia kuwa huyo Msaidizi ni Roho Mtakatifu, nafsi ya pili ya Mungu.  Hivyo ndivyo walivyofundishwa Kanisani na mapadri.  Imani hii yazidi kutiliwa nguvu na hiyo kauli "huyo roho Mtakatifu" iliotiwa kati baada ya neno "Msaidizi" liliomo katika mstari wa 26 sura ya 14 ya hii Injili ya Yohana. Hapana lawama basi kuwa baadhi yetu tukawa tunaamini kuwa Yesu ametwambia katika Yohana 14 na 16 kuwa atakuja Roho Mtakatifu ndiye atayetuongoza na kutufundisha yote yaliyobaki sisi kufunzwa, na ambayo yeye Yesu hakuwa na wakati kufundisha au watu wakati ule walikuwa bado hawajawa tayari kuyapokea.

Kwa kuwa Roho Mtakatifu anaongoza Kanisa la Yesu (yaani ndio Mapadri, tangu Baba Mtakatifu mpaka Maaskofu na Mapadri wote, na Wazee wa Kanisa,  na Wachungaji) ndio Wakristo hawana wasiwasi wala hawajiulizi kwa nini leo wanafundishwa mambo ambayo Yesu hakuyafundisha, na wanapewa amri, au kukatazwa jambo, ambalo Yesu hakuliamrisha au hakulikataza. Roho Mtakatifu ni Nafsi ya Mungu, ni sawa sawa na Yesu, basi ana madaraka kuendelea kufunza, kuamrisha na kukataza, kama Yesu, Mungu Mwana, na Mwenyezi Mungu, Mungu Baba.  Yesu alionekana na watu walimwona. Alisema na maneno yake yameandikwa. Lakini Roho Mtakatifu ananon'gona na Mapadri tu na Wakristo wanafuata wanayoambiwa na Kanisa, yaani Mapadri.

Si ajabu kuona wanaojiita Wakristo wanafuata Kanisa zaidi kuliko kumfuata Yesu Kristo mwenyewe kwa sababu wamejazwa katika akili zao kuwa nafsi ya pili ya Mungu ipo Kanisani ikiendeleza kuugeuza Ukristo wa Yesu kama ipendavyo hiyo nafsi.

Lakini natuyazingatie haya:
Kwa mujibu wa imani ya Kanisa, Roho Mtakatifu ni Mungu, ambaye ni sawa na Mungu Baba, na Mungu Mwana.  Tumeona katika maneno ya Yesu kuwa Msaidizi atakuja baada yake Yesu, yaani wakati huo hakuwako. Je, tuseme kuwa wakati wa Yesu hakuwako Mungu Roho Mtakatifu?  Mbali ya kuwa Roho ameelezwa mara nyingi sana katika Agano la Kale, na kuwa ndio akiwaongoza manabii wote, bali Wakristo wanaamini kuwa waandishi wote wa vitabu vya Biblia, kabla na baada ya Yesu, waliongozwa na Roho Mtakatifu. Tunasoma humu humu katika Injili ya Yohana sura ya kwanza mstari wa 32:
Tena Yohana akashuhudia akisema, Nimemwona Roho akishuka kama hua kutoka mbinguni;  naye akakaa juu yake (Yesu).
Yohana 1.32

Tena tunasoma katika Injili ya Marko:
Mara Roho akamtoa (Yesu) aende nyikani.
Marko 1.12

Na tunaona katika Luka:
Kwa sababu atakuwa mkuu mbele za Bwana; hatakunywa divai wala kileo;  naye atajazwa Roho Mtakatifu hata tangu tumboni mwa mamaye.  Na wengi katika Waisraeli atawarejeza kwa Bwana Mungu wao.
Luka 1.15-16

Roho Mtakatifu daima dawamu yu pamoja na Yesu, hangojei kuondoka kwake ndio aje. Alikuwa na Yohana Mbatizaji (Nabii Yahya) tangu tumboni mwa mamaake.  Luka hapo anatupa ushahidi kuwa Yohana hakupata kunywa divai wala kileo "kwa sababu atakuwa mkuu mbele ya Mungu”. 

Ni nani, basi aliyewahalalishia Wakristo kunywa ulevi, hata ikawa ibada yao haitimii ila wanywe mvinyo?  Labda ni Paulo akiongozwa na Roho Mtakatifu. Ni kweli wafuasi wa kweli wa Yesu sio wale wapigao kelele, Bwana, Bwana, sisi twaamini uwokozi wa damu yako. Wafuasi wake wa kweli ni wale wanaotenda aliyofundisha, na wanaokwenda mwendo wake. Hao hata hawana haja ya kujiita Wakristo.

Si kama Roho Mtakatifu alikuwa na Yesu tangu tumboni mwa mamaake tu kama Yohana, bali tunaambiwa na Injili ya Mathayo kuwa hiyo mimba yenyewe kaichukua mama yake, Mariamu, "
kwa uweza wa Roho Mtakatifu." (Mathayo 1.18).

Ni wazi kabisa kuwa Roho Mtakatifu hakungojea Yesu aondoke ndio aje, bali daima milele yupo, kwa ushahidi wa Biblia yenyewe. Kwa ushahidi huu tu tunayakinika kuwa huyo Msaidizi ajaye, siye Roho Mtakatifu, nafsi ya pili ya Mungu.

Tena tunaambiwa kuwa Roho Mtakatifu ndiye anayeongoza Kanisa mpaka hii leo. Lifanywalo na lisemwalo na Kanisa basi ni kwa uwongozi na ufunuo wa Roho Mtakatifu, huyo aliyebashiriwa na Yesu kama ilivyosimuliwa katika Injili ya Yohana. Lakini ilivyokuwa Ukristo ulivyogawika katika makanisa, au madhehebu, yasiokuwa na hisabu, na kila kanisa linafunza mambo ambayo tangu msingi wake yanakhitalifiana na mengineyo, jee ni madhehebu gani, au kanisa gani, linaloongozwa na Roho Mtakatifu.

Kama wote hao wanaongozwa na Roho huyo huyo basi mbona wanagongana katika mambo ya msingi? Bali hata kanisa moja, mathalan, Kanisa Katoliki la Roma, ndilo kubwa lao na lenye nidhamu kuliko yote, mbona mara ny
ingi hugeuza geuza maoni yake? 

Zamani tulipokuwa wadogo ilikuwa mwiko kwa Wakatoliki kula nyama siku ya Ijumaa, kwa kuwa ndio siku aliyotundikwa Bwana Yesu. Sasa ni halali. Zamani ilikuwa mwenye kuwa na wake zaidi ya mmoja akitengwa, na wala hapati ibada fulani za sakramento, kama Kushiriki katika Chakula cha Bwana.  Leo wanakubaliwa, na inakubaliwa kuwa kuoa mke mmoja si sharia ya Kikristo bali ni mila za Kizungu zilizoingizwa katika dini. Aliyewazindua Wazee wa Kanisa ni Roho Mtakatifu?  Ikiwa ni yeye kwa nini huyo Roho Mtakatifu alinyamaza kimya miaka yote hiyo? Wangapi waliotengwa na Kanisa, wakalaaniwa, na wakachomwa moto hadharani, na baadae watu hao hao baada ya miaka kupita wakaja wakatakaswa na kubarikiwa na kutangazwa na Kanisa lile lile kuwa niWatakatifu? Na wakati huo huo tuone ni Roho Mtakatifu, Mungu, asiyekosea, ndiye amelijaa Kanisa na analiongoza!  Bila ya shaka huyu siye aliyebashiriwa na Yesu.

Kanisa la Roma linasema ni haramu kwa padri kuoa. Hivi sasa wapo mapadri si chini ya 80,000 duniani wa Kanisa la Roma ambao wana wake, miongoni mwao 18,000 wako Amerika (U.S.A.). Si ajabu kutokea siku yo yote kuwa Baba Mtakatifu, huku akiongozwa na Roho Mtakatifu, akiona mambo ni ya mno, akatoa amri kuwa sasa ni halali kwa mapadri kuoa bila ya kificho, na bila kuleta nuksani yo yote.

Yesu ametwambia kuwa huyo ajaye hatanena kwa shauri lake mwenyewe. Je, Roho Mtakatifu, ambaye ni Mungu, hunena kwa shauri ya nani?  Mungu hunena anayoyasikia au hunena yake mwenyewe? Ikiwa hunena anayoyasikia, basi anayasikia kwa nani? Kwa Mungu Baba, au kwa Mungu Mwana, na hali tunaambiwa katika Utatu, nafsi zote tatu ni sawa.   Ikiwa yeye ni Roho Mtakatifu, ambaye ni Mungu, pana lipi la ajabu hata ihitajie Yesu kusema kuwa atatoa habari ya mambo yajayo? Hapana ajabu Mungu kuagua yajayo, na hali ni Yeye aliyeyaumba.

Huyo ajaye, Yesu anasema, atamtukuza Yesu. Kwani Mungu Mwana ana haja gani ya kutukuzwa na Mungu Roho?

Hayo yote tukiyazingatia kwa nia safi tutaona kuwa hayamuelekei Roho Mtakatifu, ambaye ni Mungu kama lisemavyo Kanisa, hata chembe.  Je, kama bishara hii haimuelekei Roho Mtakatifu, inamuelekea nani?  Ni mtu gani huyo ambaye alikuja ulimwenguni baada ya kuondoka Yesu, akauhakikisha ulimwengu kwa khabari ya dhambi na hukumu, akauongoza ulimwengu na kuutia kwenye kweli yote, akawa haneni kwa shauri lake wala mapenzi yake bali husema kwa aambiwayo na Mwenyezi Mungu, akatoa khabari ya dhambi na mambo yajayo, akatwachia mafunzo katika Kitabu kisichobadilika milele na mafunzo yake yakakaa nasi milele mpaka mwisho wa dunia, akamtukuza Yesu Kristo?  Katika historia yote hakutokea mtu mwenye kukusanya sifa zote hizo ila Nabii Muhammad tu.

Mtume Muhammad s.a.w. ndiye aliyekuja baada ya Nabii Isa a.s. Yeye peke yake katika Manabii na Mitume wote ndiye aliyesema maneno ya kutimiza ujumbe wote wa Mwenyezi Mungu, ndiye aliyeleta kweli yote.  Kila Nabii aliyetangulia alibashiri kuja mwinginewe baadae. Musa alisema hayo, na Yesu kasema hayo, na wenginewe wote wamesema.  Ila Nabii Muhammad ndiye aliyesema: "
Hapana Nabii baada yangu."  Na Mwenyezi Mungu alimwambia karibu ya kufa kwake:
Leo waliokufuru wamekata tamaa katika Dini yenu, basi msiwaogope, bali niogopeni Mimi.  Leo nimekukamilishieni Dini yenu, na nimekutimizieni neema yangu, na nimekupendeleeni Uislamu uwe ndiyo Dini.
Qur’an Al Maida 5:3

Mwenye kukamilishiwa Dini na kutimiliziwa Neema, amekamilishiwa na kutimiliziwa kila kitu: ndiyo kweli yote, na hukumu na khabari ya dhambi.  Ni Muhammad ndiye ambaye alikuwa akijuulikana hata na maadui wake kuwa ni msema kweli, wa kuaminiwa, Assaadiq, Al Amin, "Mkweli Muaminifu" na kweli ndiye Roho wa kweli.
Huyo ajaye, Yesu anatwambia, hatanena kwa shauri lake.  Ni Mtume Muhammad, peke yake, ndiye ambaye historia inatwambia kuwa mafunzo yake ni maneno ya Mwenyezi Mungu.
Qur’an Tukufu yote ni maneno ya Mungu, moja kwa moja.  Qur’an haikutungwa na Muhammad wala na ye yote katika wanaadamu.  Sio kama vitabu vya Biblia, ambavyo vinajuulikana vimeandikwa na watu fulani kama vile Injili ya Mathayo, ya Marko n.k. na Torati ya Musa.  Hii ni Qur’an ya Mwenyezi Mungu, si ya Muhammad.  Kama isemavyo hiyo Qur’an:
Arrahman (Mwingi wa Rehema) amefundisha Qur’an.
Qur'an Arrahman 55.1-2

Na ilivyobainishwa katika Sura An Najm:
Wala (Muhammad) hasemi kwa matamanio. Hayakuwa haya ila ni ufunuo uliofunuliwa;  amemfundisha Mwenye nguvu kweli.
Qur’an Annajm 53.3-5

 Na ilivyosemwa katika Sura An Nisaa:
Hawaizangatii Qur’an? Na lau kama imetoka kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu bila ya shaka wangelikuta ndani yake khitilafu nyingi.
Qur’an An Nisaa 4.82

Mkristo wa Kiingereza, Dr. John B. Taylor, Mwalimu wa Masomo ya Kiislamu katika Chuo cha Birmingham, ameandika katika kitabu chake: Thinking About Islam (Kuufikiria Uislamu):
"Tumethibitisha ya kuwa Waislamu hawasemi kuwa Muhammad ndiye aliyeandika Qur’an, lakini kuwa yeye ameipokea na akaisoma.  Kama alivyokuwa Muhammad mwenyewe akishughulika mno kuyaweka safi maandiko (matini) ya Qur’an, basi hali kadhaalika wale  Waislamu waliokuja baada yake walifanya juhudi kuhifadhi bila ya kukosea ko kote vipande mbali mbali vya Qur’an.  Miaka miwili tu baada ya kufa Muhammad, kwa kuwa walikufa vitani baadhi ya wale waliokuwa wameihifadhi kwa moyo, sehemu mbali mbali za Qur’an zilikusanywa...
"Baada ya miaka michache, katika enzi ya Uthman, Khalifa wa tatu kuwatawala Waislamu baada ya Muhammad, ilipitiwa mara ya mwisho kusahihishwa matini ya Qur’an.  Twaweza kutambua vipi walivyokuwa na hadhari kubwa wale Waislamu wa mwanzo kwa vile hata kukhitalifiana matamshi baina ya sehemu moja ya nchi za Kiislamu na nyengine, hakukuruhusiwa.  Kwa hivyo yale maandishi ya rasmi yakathibitishwa kufuata lafdhi ya Makka, na zile ziliobaki zikateketezwa kwa amri ya Khalifa.  Kwa hivyo tunaweza kuwa na yakini kuwa hii Qur’an tulio nayo hii leo, kama iwezekanavyo kibinaadamu, ndio ile ile iliyothibitishwa miaka michache tu baada ya kufa Mtume."

Hayo ni maneno ya Mkristo ambaye kazi yake ni kuutafutia ila na nuksani Uislamu. 
Qur’an ni neno la Mwenyezi Mungu lisio na upungufu wo wote kwa sababu ni maneno yake mwenyewe.  Hayo ndiyo makusudio ya Yesu aliposema kuwa huyo Msaidizi ajaye, "hatanena kwa shauri lake mwenyewe." 

Yesu kadhaalika ametwambia kuwa Msaidizi atakayekuja atatoa khabari ya mambo yajayo. Kila alilosema Mtume Muhammad s.a.w. kuwa litakuja basi limetokea vile vile alivyosema.  Katika alilosema ni kuwa Warumi baada ya kushindwa na Waajemi wao watakuja shinda mnamo miaka michache na hapo Waislamu watafurahi. Na kweli walishindwa Waajemi mwaka 624 B.K. na ndio mwaka Waislamu walipowashinda makafiri wa Kikureshi katika vita vya Badru.

Mtume alipokubali mkataba wa suluhu pale alipozuiliwa kuingia Makka alisema kuwa Waislamu watakuja kuikomboa Makka karibuni, na hakika hivyo ndivyo ilivyokuwa baada ya miaka miwili, na ikawa ndio ushindi ulioenea Arabuni kote.

Mtume Muhammad alipokuwa akichimba handaki, pamoja na Masahaba zake, kuilinda Madina na maadui, kulimetuka cheche tatu alipokuwa akipiga mtaimbo kulisukua jiwe.

Cheche moja ilielekea kusini, Mtume akasema Yaman itasilimu. Cheche ya pili ikaelekea mashariki, na Mtume akasema Iran itasilimu. Cheche ya tatu ilipometukia kaskazini Mtume s.a.w. akasema Sham iliyokuwa chini ya utawala wa Kikristo wa Kirumi itasilimu. 

Na zote zikaja kusalimu amri na kusilimu hivyo hivyo kama alivyobashiri, kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu, katika zama ambazo Warumi walikuwa ndio kama Marekani walivyo sasa, na Waajemi ndio kama Warusi walivyo sasa. Hizo ndizo dola kubwa kabisa, na Muhammad ni bedui mnyonge ambaye ndiye kwanza kachipuka huko jangwani akiwahubiria makafiri wa miji miwili midogo kabisa Makka na Madina.  Na mengi, kabisa, aliyokuwa akiyasema Mtume Muhammad s.a.w. na yote yalikuwa hayaanguki chini. 

Nimeyataja hayo ambayo yamo katika vitabu vya historia vilivyoandikwa hata na wasiokuwa Waislamu.

Yesu tena amesema huyo Msaidizi "
atanitukuza mimi."  Na kweli Yesu Kristo au Isa Masihi (wamuitavyo Waislamu) alitukanwa na  maadui zake, Mayahudi, kwa kumwambia kuwa ati ni mwana haramu, mzushi, mlaanifu.  Wakidai kuwa uthibitisho wa laana hiyo ni kuwa waliweza kumwua kwa kumtundika msalabani.

Taurati ilisema kuwa ye yote anayekufa kwa kutundikwa kwenye mti basi amelaanika, na hayo ndiyo yalikuwa makusudio yao. Hali kadhaalika waliokuwa wakijiona kuwa ni wafuasi wake Yesu watiifu walimvunjia daraja yake kwa kukubali madai ya Mayahudi kwa kuwa alikufa msalabani, na pia kwa kumfanya yeye ni sawa na ile miungu ya bandia ya uwongo sawa na ya akina Mithra, na Apollo, na Osiris ya kipagani, na kwa kumtoa kwenye cheo chake kitukufu ambacho yeye mwenyewe alikuwa akitafakhari nacho kama isemavyo Biblia.

Daima Yesu akitafakhari na kujiita yeye ni mwanaadamu, mtumishi wa Mwenyezi Mungu, ambaye hawezi kusema kitu wala kutenda kitu ila kama anavyoamrishwa na Mungu. Yesu akitafakhari kuwa ni Nabii wa Mwenyezi Mungu, na Mtume wake, sio kuwa mungu kama miungu iliyojaa katika pande zile kwa zama zile. Hata wafalme madhaalimu wa Kirumi walikuwa wakiitwa miungu.  Wao hao wajiitao Wakristo waliacha kufuata mafundisho yake Yesu na kuyatenda, na badala yake wakafuata mafundisho ya wale wale washirikina ambao Yesu kaja kuwapinga.  Ndio maana akasema: 
"Wengi watanambia  siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi?  Ndipo nitwaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu."
Ni kwa kupitia Mtume Muhammad, huyo Msaidizi aliyetwambia Yesu kuwa atakuja kumtukuza, ndio tunasoma maneno ya
Qur’an Tukufu:

Enyi watu wa Kitabu Msipite kiasi katika dini yenu, wala msiseme juu ya Mwenyezi Mungu ila yaliyo kweli.  Hakika Masihi, Isa bin Maryam, ni Mtume wa Mwenyezi Mungu na neno lake alilompelekea Maryam, na ni roho iliyotoka kwake. Basi mwaminini Mwenyezi Mungu na Mitume yake; wala msiseme, "Watatu".  Wacheni! Itakuwa kheri kwenu.  Bila shaka Mwenyezi Mungu ni Mungu mmoja tu.  Ametakasika Yeye kuwa na mwana. Ni vyake vilivyomo mbinguni na vilivyomo duniani;  na Mwenyezi Mungu ni mtegemewa wa kutosha.  Masihi hataona uvunjifu kuwa mtumwa wa Mwenyezi Mungu, wala Malaika waliokurubishwa.  Na watakaouona uvunjifu utumwa wa Mungu na kufanya kiburi, basi atawakusanya wote kwake.
Qur’an An Nisaa 4.171-172

Katika Sura Al Imran tunasoma vipi alivyotukuzwa Yesu:
Waliposema Malaika: Ewe Maryam!  Mwenyezi Mungu anakubashiria kwa neno litokalo kwake, jina lake ni Masihi Isa, mwana wa Maryam, mwenye hishima katika dunia na Akhera, na miongoni mwa waliokaribishwa (kwa Mungu). Naye atazungumza na watu katika utoto wake na katika utuuzima wake, na atakuwa katika watu wema.  (Maryam) akasema: Mola wangu!  Vipi nitampata mtoto na hali hajanigusa mwanaadamu ye yote?  Akasema: Ndivyo vivyo hivyo, Mwenyezi Mungu huumba apendacho; anapohukumu jambo, huliambia: Kuwa, basi huwa.  Na atamfunza Kitabu na Hikima na Taurati na  Injili.  Na ni Mtume kwa wana wa Israili.
Qur’an Al Imran 3.45-49

Na kabla ya aya hizi inasimuliwa vipi alivyoteuliwa mama yake Yesu na kutukuzwa:

Na Malaika waliposema: Ewe Maryam, kwa hakika Mwenyezi Mungu amekuteuwa na kakutukuza kuliko wanawake wa ulimwengu.
Qur’an) Al Imran 3.42

0 comments/Maoni: